Wednesday, July 10, 2013

WAANDISHI WA HABARI MKOANI RUVUMA WATAKIWA KUANDIKA HABARI KWA KUZINGATIA WELEDI

Na Nathan Mtega,Mbinga
 
 WAANDISHI wa habari mkoani Ruvuma wametakiwa kuandika na kutangaza habari mbali mbali kwa kuzingatia maadili ya kazi yao na kujiepusha na habari za uchochezi,ubaguzi na zinazochochea mifarakano katika jamii kwa sababu jamii ina imani kubwa na wanahabari hasa wanaofanya kazi yao kwa kuzingatia weledi na maadili ipasavyo.
 
 Wito huo umetolewa na mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma Allanus  Ngai wakati akifunga kikao cha dharula cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo kilichofanyika bada ya uchaguzi wa mwenyekiti na makamu mwenyekiti ambao awali uliahirishwa baada ya jina la mwenyekiti huyo kuenguliwa katika mazingira ya kutatanisha na kusababisha mtafaruku ndani ya halmashauri hiyo.
 
Alisema kuwa katika tukio hilo la kuenguliwa kwa baadhi ya majina ya wagombea kwa ajili ya kundi moja kupanga safu yta uongozi ndani ya halmashauri kwa manufaa yao waandishi wa habari mkoani Ruvuma walionyesha moyo wa uzalendo kwa kutafuta ukweli na kuufanyia kazi kwa ajili ya maslahi ya walio wengi na hawakuonyesha upendeleo wa aina yoyote katika kuitafuta haki hiyo ya wanyonge ambayo hatimaye imepatikana.
 
Aidha alitoa pongezi kw waandishi wa habari huku akiwaasa kuepuka kutumiwa na baadhi ya viongozi au kundi la watu ambalo lipo kwa ajili ya maslahi binafsi kwa kuwatumia baadhi ya waandishi wa habari wasio waadilifu kujinufaisha na kuendelea kuwadhulumu wanyonge walio wengi lakini katika tukio hilo la uchaguzi wa viongozi wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga waandishi wa habari wameonyesha  ukomavu wao na wanastahili pongzei.
 
Alisema kuwa waandishi wa habari waliandika na kutangaza ukweli kuhusu mchakato mzima wa uchaguzi huo kwa kuwataja wahusika wa kupanga safu ya uongozi ndani ya halmashauri hiyo kwa maslahi ya kundi fulani  na kusababisha uchaguzi kusitishwa na hatimaye ukweli huo umezaa matunda kwa jamii ya watu wa Mbinga.
 
  Katika hatua nyingine mwenyekiti huyo amewaagiza wakuu wa idara zote ndani ya halmashauri hiyo kutoa ushirikiano mkubwa kwa waandishi wa habari na vyombo vya habari viweze kutangaza fursa za maendeleo zilizopo ndani ya halmashauri hiyo na hatua zitachukuliwa dhidi ya mkuu wa idara ambaye atathibitika kutoto ushirikiano kwa wanahabari kwa maslahi au sababu binafsi.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...