Friday, July 5, 2013

DANGURO LA WAVUTA BANGI NA DAWA ZA KULEVYA TABATA

NYUMBA iliyogeuzwa danguro la vijana kuvutia bangi na kufanyia ufuska imenaswa maeneo ya Tabata-Shule jijini Dar.
Kwa mujibu wa wananchi waishio maeneo hayo, wamekuwa wakikerwa na vitendo vya kifuska vinavyofanyika katika nyumba hiyo inayodaiwa kumilikiwa na mwanamke aliyefahamika kwa jina la Deograsia Nchimbi.


Baada ya wananchi hao kutoa malalamiko kwa mama huyo mara kwa mara bila mafanikio, waliamua kukitaarifu kikosi kazi cha waandishi ili waweze kufanya kazi yao.

“Kwa kweli tumesema hadi tumechoka huyu mama amekuwa chanzo cha kuharibu tabia vijana wetu, nyumba yake imekuwa kero

.

“Ngono zembe zinafanyika waziwazi bila hata ya kificho, hata sijui tunakipeleka wapi hiki kizazi cha sasa!” alisema mkazi wa eneo hilo aliyeomba hifadhi ya jina.

Baada ya kupokea taarifa hizo, kikosi kazi maarumu, kiliingia mzigoni na kufanya uchunguzi, kilipobaini ukweli ndipo kilipolitaarifu Jeshi la Polisi, Buguruni kisha kuvamia.


Kikosi kazi cha waandishi wa habari na polisi walivamia katika nyumba hiyo hivi karibuni majira ya saa kumi na mbili jioni na kuwakuta vijana hao wakiwa na bangi lakini mama mwenye nyumba hakukutwa na kidhibiti.

Ndani ya nyumba hiyo walikutana na vijana wasiopungua kumi lakini waliposikia mlango unafunguliwa walitimka na kuiacha misokoto ya bangi sebuleni ambapo polisi walifanikiwa kumkamata Amosi Nchimbi aliyedaiwa kuwa ni mtoto wa mama mwenye nyumba pamoja na wasichana wawili.


Baada ya purukushani ya hali ya juu kati ya polisi na vijana hao waliodaiwa kugeuza nyumba hiyo kuwa danguro, walifanikiwa kuwatia mbaroni wasichana wawili na mtoto huyo wa mwenye nyumba ambapo hadi waandishi wanaondoka eneo hilo, iliwaacha polisi wakiwa katika harakati za kuwapeleka watuhumiwa Kituo cha Polisi cha Buguruni.
Wananchi pamoja na diwani wa mtaa huo, Mtumwa Mohamed walifurahi kuona vijana hao wakipelekwa polisi kwani hali hiyo ilikuwa ikiharibu tabia za vijana wao kwa muda mrefu hivyo kuishukuru GPL kwa jitihada zake za kufichua maovu katika jamii.
“Nawashukuru kwa kweli hapa palikuwa ni kama chaka la maovu nadhani sasa hali hii itatulia. Hili eneo lilikuwa linaleta picha mbaya kabisa katika jamii,” alisema Mtumwa
 

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...