Thursday, August 1, 2013

JAMII YATAKIWA KUSHIRIKIANA KUONDOA UNYANYASAJI WA KIJINSIA KWA WATOTO WA KIKE


 Mke wa Rais Mama Salma Kikwete akikaribishwa rasmi kwenye mkutano wa "High Level Group" na Dr. Sheila Tlou, Mkurugenzi wa UNAIDS Regional Support Team kwa nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika katika siku ya pili ya mkutano huo unaofanyika jijini Gaborone nchini Botswana tarehe 31 Julai 2013.


 Mke wa Rais na Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo Mama Salma Kikwete akifunga rasmi mkutano wa High Level Group uliokuwa unafanyika kwenye hoteli ya Lasmore nchini Botswana tarehe 31 Julai 2013.
 
Mke wa Rais Mama Salma Kikwete akifanya mazungumzo na Profesa Alaphia Wright, Mwakilishi wa UNESCO kwenye nchi za ukanda wa Kusini mwa Afrika mwishoni mwa mkutano wa siku mbili wa High Level Group ulikuwa ukifanyika jijini Gaborone nchini Botswana tarehe 31 Julai 2013.
Baadhi ya wajumbe wa mkutano wakisoma jarida linalochapishwa na Taasisi ya Wanawake na Maendeleo, WAMA, huku wakiendelea na mkutano.

Na Anna Nkinda- Gaborone,  Botswana
1/8/2013 Jamii imetakiwa kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha kuwa  hakuna unyanyasaji wa kijinsia kwa watoto wa kike pia inawalinda ili wasiingie katika mazingira hatarishi yatakayowapelekea kupata  kupata maambukizi ya Virusi vya Ugonjwa wa Ukimwi (VVU) .
Wito huo umetolewa jana na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati akiongea na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa kamati maalum ya viongozi wanaoshughulikia huduma na elimu ya afya ya uzazi na ujinsia kutoka nchi za Jumuia ya Afrika ya Mashariki (EAC) na Jumuia ya Ushirikiano wa Maendeleo ya Kikanda kwa nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika  katika Hoteli ya Lansmore Masa Square iliyopo mjini Gabarone nchini Botswana.
Mama Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema  huwa anajisikia uchungu pale anaposikia  kuwa mtoto wa kike amebakwa au amefanyiwa ukatili wa kijinsia na kuiomba jamii nzima iweze kumsaidia na kumkomboa mwanamke.
“Kama jamii yetu ya nchi za kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika itaungana kwa pamoja na kuamua  kumsaidia mtoto wa kike itawezekana  kwani hata kama watoto hawa wakipata huduma bora ya afya  bila ya kuwapatiwa elimu hakuna jambo la maana watakalolifanya  kwakuwa  watakuwa na afya bora  lakini watakosa kujiamini kwani hawana elimu”, alisema Mama Kikwete.
Akiongelea kuhusu Taasisi ya WAMA alisema kitaaluma yeye ni mwalimu na wakati anafundisha aliona changamoto mbalimbali zinazowakabili watoto wa kike na pale alipoanzisha taasisi hiyo aliamua kuwasaidia watoto wa kike ambao ni yatima na wanaoishi  katika mazingira hatarishi ambao wamekosa nafasi ya kwenda shule ili nao waweze kusoma kama watoto wengine.
Mama Kikwete alisema, “ Tuna shule ya Sekondari ya Wasichana ya Mfano ya WAMA-Nakayama ambayo ina jumla ya wanafunzi 325 wa kidato cha kwanza hadi cha nne pia  Taasisi ya WAMA inawagharamia masomo wanafunzi wasichana 300 ambao wanasoma shule mbalimbali za Sekondari katika mikoa yote ya Tanzania.
Alimalizia kwa kuiziomba nchi wanachama wa EAC na SADC kutunga na kufuata sera na sheria zitakazomlinda mtoto wa kike kwa kufanya hivyo ataepukana na unyanyasaji wa kijinsia ikiwemo ubakwaji, udhalilishwaji, kutopewa huduma bora za afya na elimu.
Mkutano huo wa siku mbili uliandaliwa  na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kupamba na Ukimwi (UNAIDS) , UNFPA, Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia watoto (UNICEF), Shirika la Chakula Duniani (WHO), Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Sayansi na Utamaduni (UNESCO) lengo kuu likiwa ni  kuhakikisha kuwa vijana wote wanapata elimu kuhusiana na afya ya uzazi na ujinsia na stadi za maisha jambo ambalo litawasaidia kufahamu zaidi  ugonjwa wa Ukimwi.SOURCE:IPSHA MEDIA

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...