Saturday, October 5, 2013

LUKUVI AONGOZA MAZIKO YA DADA YAKE FREEMAN MBOWE

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge,William Lukuvi, ameongoza mamia ya waombolezaji katika mazishi ya aliyekuwa mwanamke wa kwanza nchini kusajiliwa na Bodi ya Wahandisi, Grace Aikael Mbowe (57), ambaye ni dada wa Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
 
Wakati, Lukuvi akiongoza waombolezaji kwa niaba ya Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda, Mbunge wa Moshi Mjini (Chadema), Philemon Ndesamburo alisimama wakati wa kutoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Dk.Wilbrod Slaa na kuwaonya waombolezaji na viongozi wa vyama vya siasa waliojitokeza msibani kutothubutu kutumia msiba huo kama sehemu ya kuhubiri siasa na badala yake waonyeshe upendo wao katika kuwatia nguvu wafiwa
.
Akitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Lukuvi alisema serikali imepokea msiba huo kwa masikitiko makubwa na kwamba ofisi yake inaungana na familia ya Freeman Mbowe katika kipindi kigumu inachopita kwa sasa.

Grace alifariki katika ajali ya gari wiki iliyopita katika eneo la Kabuku,Wilaya ya Handeni, mkoani Tanga wakati akielekea jijini Dar es Salaam.

Alikuwa mwanamke wa pili kusajiliwa na bodi ya wahandisi nchini akiwa kama Ofisa mpimaji (Quantity Surveyer) baada ya kuhitimu elimu ya juu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,kitengo ardhi (ARU).

Lukuvi na viongozi wengine wa serikali pamoja na Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi na wabunge kadhaa wa Chadema, waliongoza waombolezaji kumzika Grace katika makaburi ya familia, Kijiji cha Nshara-Lambo,Tarafa ya Machame Wilaya ya Hai.

Katika mazishi hayo yaliyoongozwa na Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini, Dk. Martin Shao, msemaji wa Chadema na mbunge wa jimbo la Moshi,  Ndesamburo, alisema Chadema imetoa rambirambi ya  Sh.mil. 1,000,000.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Kilimanjaro, Idd Juma, alisema kifo cha Grace kimeacha pengo kubwa katika familia ya Mbowe na kwamba hali hiyo isiwafanye watanzania wakaacha kujenga undugu walionao na badala yake kiwafanye kuwa wamoja zaidi.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...